Leo ningenda turudie mada ambayo tulikwishaiongelea hapa awali
kuhusu tofauti za kijinsia ambazo nyingi kati ya hizo zimekuwa ni kiini cha
migogoro ya hapa na pale katika maisha yetu ya ndoa.
Ziko tofauti nyingi za kijinsia kati ya wanawake na wanaume,
ambazo mara nyingi zimekuwa chanzo cha migongano, migogoro na mivutano katika
ndoa. Kutokuzifahamu tofauti hizi kumesababisha wanandoa kupeana upendo ambao
kila mmoja angependa apatiwe, badala ya upendo ambao mwenzake angependa apatiwe
yeye, kulingana na silika ya jinsia yake.
Mara nyingi wanawake wamewapa wanaume
malezi ya kuwajali, badala
ya malezi ya kuonyesha kuwa na
Imani nao. Wakati huo huo,
wanaume wamewapa wanawake malezi kuonyesha kuwa
na Imani nao, badala ya
malezi ya kuwajali.
Kutokana na mpishano huu, ndoa nyingi zimejikuta katika mivutano mingi, na
changamoto ya kutokuridhishana, kwa pande zote mbili.
Utakuta, kwa vile mahitaji ya mwanamke ya msingi ya hisia za moyo
ni mwenzi wake kumjali, basi
anafikiri ndiyo mahitaji ya msingi ya mwanaume pia. Vivyo hivyo, utakuta
mwanaume anataka mpenzi wake aonyeshe kuwa na imani naye. Hivyo, anajaribu kutoa mapenzi
ya kuonyesha kuwa na Imani kwa mwenzi wake hitaji ambalo yeye angependa apatiwe
na huyo mwenzi wake. Kila mmoja, pasipo kujua, anatoa aina ya mapenzi ambayo
yeye angependa apatiwe, badala ya mapenzi ambayo mwenzi wake angependa apatiwe,
kutokana na tofauti ya kijinsia aliyonayo.
Kwa kuelewa tofauti hizi za jinsia, na kwa kujitahidi kuuweka ufahamu
huo katika matendo, misuguano iliyoko katika ndoa kati ya wanawake na wanaume
itaweza kupungua kwa kiasi kikubwa. Ingawa hii pekee yake haitoshi kumaliza
mivutano na migogoro katika ndoa, lakini ni moja ya njia muhimu ya kuboresha
mahusiano katika ndoa.
Kuna wanandoa ambao, hata pasipo ufahamu huu, wameweza
kuchukualiana na kuishi pamoja kwa mafanikio, na kuweza kuoanisha tofauti hizi
za kijinsia. Hii ni kutokana na kipawa na alichonacho mmojawapo au wote wawili,
katika kuoanisha tofauti hizi. Lakini, kufanikiwa huku pasipokuwa na ufahamu
huu kunatokana na kipawa
cha kuzaliwa.
Lakini hata kama mtu anacho kipawa cha kuzaliwa, kukiboresha
kupitia kuongeza ufahamu ni jambo la msingi. Hata kama ndoa ni bora, siku zote
kuna nafasi ya kuzidi kuboresha zaidi na zaidi kupitia kuongeza ufahamu kuhusu
ndoa. Maarifa siku zote ni silaha. Yaani maarifa yanampa mtu uwezo wa kutawala
jambo.
Dr. Abraham Maslow, mwanasaikolojia mashuhuri wa karne ya
ishirini, anaeleza kuhusu ufahamu na maarifa, kama ifuatavyo;
Elimu, ujuzi, ufahamu, kuijua kweli, na udhihirisho ni tiba ya
hali ya juu…….na kama ufahamu
unatibu, basi kukosa ufahamu kunasababisha kuugua.
Maarifa, ufahamu, ujuzi au elimu ni silaha muhimu sana kwa
binadamu, silaha ambayo ikimpa kudhibiti mambo, na kutawala changamoto
mbalimbali katika maisha yake. Na katika ndoa pia, maarifa yanayohusu ndoa ni
moja ya mhimili muhimu.
No comments:
Post a Comment